Fermer le panneau de recherche

Appuyez sur Entrée pour rechercher ou ESC pour annuler.

Luc 4.43
Bible en Swahili de l’est


Tentation de Jésus

1 Na Yesu, hali amejaa Roho Mtakatifu, alirudi kutoka Yordani, akaongozwa na Roho muda wa siku arobaini nyikani,
2 akijaribiwa na Ibilisi. Na siku hizo alikuwa hali kitu; hata zilipotimia, aliona njaa.
3 Ibilisi akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, liambie jiwe hili liwe mkate.
4 Yesu akamjibu, Imeandikwa ya kwamba mtu hataishi kwa mkate tu.
5 Akampandisha juu, akamwonyesha milki zote za ulimwengu kwa dakika moja.
6 Ibilisi akamwambia, Nitakupa wewe enzi hii yote, na fahari yake, kwa kuwa imo mikononi mwangu, nami humpa ye yote kama nipendavyo.
7 Basi, wewe ukisujudu mbele yangu yote yatakuwa yako.
8 Yesu akajibu akamwambia, Imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake.
9 Akamwongoza mpaka Yerusalemu, akamweka juu ya kinara cha hekalu, akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, jitupe chini;
10 kwa maana imeandikwa, Atakuagizia malaika zake wakulinde;
11 na ya kwamba,mikononi mwao watakuchukua, Usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe.
12 Yesu akajibu akamwambia, Imenenwa, Usimjaribu Bwana Mungu wako.
13 Basi alipomaliza kila jaribu, Ibilisi akamwacha akaenda zake kwa muda.

Ministère de Jésus en Galilée

Jésus à Nazareth

14 Yesu akarudi kwa nguvu za Roho, akenda Galilaya; habari zake zikaenea katika nchi zote za kandokando.
15 Naye alikuwa akifundisha katika masinagogi yao, akitukuzwa na watu wote.
16 Akaenda Nazareti, hapo alipolelewa; na siku ya sabato akaingia katika sinagogi kama ilivyokuwa desturi yake, akasimama ili asome.
17 Akapewa chuo cha nabii Isaya, akakifungua chuo, akatafuta mahali palipoandikwa,
18 Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa,
19 Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa.
20 Akakifunga chuo, akamrudishia mtumishi, akaketi; na watu wote waliokuwamo katika sinagogi wakamkazia macho.
21 Akaanza kuwaambia, Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu.
22 Wakamshuhudia wote, wakiyastaajabia maneno ya neema yaliyotoka kinywani mwake, wakasema, Huyu siye mwana wa Yusufu?
23 Akawaambia, Hapana shaka mtaniambia mithali hii, Tabibu, jiponye nafsi yako; mambo yote tuliyosikia kwamba yametendeka Kapernaumu, yatende na hapa pia katika nchi yako mwenyewe.
24 Akasema, Amin, nawaambia ya kwamba, Hakuna nabii mwenye kukubaliwa katika nchi yake mwenyewe.
25 Lakini, kwa hakika nawaambia, Palikuwa na wajane wengi katika nchi ya Israeli zamani za Eliya, wakati mbingu zilipofungwa miaka mitatu na miezi sita, njaa kuu ikaingia nchi nzima;
26 wala Eliya hakutumwa kwa mmojawapo, ila kwa mjane mmoja wa Sarepta katika nchi ya Sidoni.
27 Tena, palikuwa na wenye ukoma wengi katika Israeli zamani za nabii Elisha, wala hapana aliyetakaswa ila Naamani, mtu wa Shamu.
28 Wakajaa ghadhabu wote waliokuwa katika sinagogi walipoyasikia hayo.
29 Wakaondoka wakamtoa nje ya mji, wakampeleka mpaka ukingo wa kilima ambacho mji wao umejengwa juu yake, wapate kumtupa chini;
30 lakini yeye alipita katikati yao, akaenda zake.

Miracles à Capernaüm

31 Akashuka mpaka Kapernaumu, mji wa Galilaya, akawa akiwafundisha siku ya sabato;
32 wakashangaa mno kwa mafundisho yake, kwa kuwa neno lake lilikuwa na uwezo.
33 Na ndani ya sinagogi mlikuwa na mtu mwenye roho ya pepo mchafu, akalia kwa sauti kuu,
34 akisema, Acha! Tuna nini nawe, Yesu wa Nazareti? Umekuja kutuangamiza? Nakujua u nani, Mtakatifu wa Mungu.
35 Yesu akamkemea, akisema, Fumba kinywa, mtoke. Ndipo yule pepo akamwangusha katikati, akamtoka asimdhuru neno.
36 Mshangao ukawashika wote, wakasemezana wakisema, Ni neno gani hili, maana awaamuru pepo wachafu kwa uwezo na nguvu, nao hutoka.
37 Habari zake zikaenea kila mahali katika nchi ile.
38 Akatoka katika sinagogi, akaingia katika nyumba ya Simoni. Naye mkwewe Simoni, mamaye mkewe, alikuwa ameshikwa na homa kali, wakamwomba kwa ajili yake.
39 Akasimama karibu naye, akaikemea ile homa, ikamwacha; mara hiyo akaondoka, akawatumikia.
40 Na jua lilipokuwa likichwa, wote waliokuwa na wagonjwa wenye maradhi mbali mbali waliwaleta kwake, akaweka mikono yake juu ya kila mmoja akawaponya.
41 Pepo nao waliwatoka watu wengi, wakipiga kelele na kusema, Wewe u Mwana wa Mungu. Akawakemea, asiwaache kunena, kwa sababu walimjua kuwa ndiye Kristo.
42 Hata kulipokucha alitoka akaenda mahali pasipokuwa na watu; makutano wakawa wakimtafuta-tafuta, wakafika kwake, wakataka kumzuia asiondoke kwao.
43 Akawaambia, Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana kwa sababu hiyo nalitumwa.
44 Basi, alikuwa akihubiri katika masinagogi ya Galilaya.

Cette Bible est dans le domaine public.