Fermer le panneau de recherche

Appuyez sur Entrée pour rechercher ou ESC pour annuler.

Genèse 21.9
Bible en Swahili de l’est


Naissance d’Isaac et départ d’Ismaël

1 Bwana akamjia Sara kama alivyonena, na Bwana akamfanyia kama alivyosema.
2 Sara akapata mimba akamzalia Ibrahimu mwana wa kiume katika uzee wake, kwa muhula alioambiwa na Mungu.
3 Ibrahimu akamwita jina lake Isaka, yule mwana aliyezaliwa, ambaye Sara alimzalia.
4 Ibrahimu akamtahiri Isaka mwanawe, alipokuwa mwenye siku nane, kama Mungu alivyomwamuru.
5 Naye Ibrahimu alikuwa mtu wa miaka mia, alipozaliwa mwana wake Isaka.
6 Sara akasema, Mungu amenifanyia kicheko; kila asikiaye atacheka pamoja nami.
7 Akasema, N’nani angemwambia Ibrahimu, Sara atanyonyesha wana? Maana nimemzalia mwana katika uzee wake.
8 Mtoto akakua, akaachishwa kunyonya; Ibrahimu akafanya karamu kuu siku ile Isaka alipoachishwa kunyonya.
9 Sara akamwona yule mwana wa Hajiri Mmisri, ambaye alimzalia Ibrahimu, anafanya dhihaka.
10 Kwa hiyo akamwambia Ibrahimu, Mfukuze mjakazi huyu na mwanawe, maana mwana wa mjakazi hatarithi pamoja na mwanangu, Isaka.
11 Na neno hilo lilikuwa baya sana machoni pa Ibrahimu, kwa ajili ya mwanawe.
12 Mungu akamwambia Ibrahimu, Neno hili lisiwe baya machoni pako, kwa ajili ya huyo mwana, na huyo mjakazi wako. Kila akuambialo Sara, sikiza sauti yake, kwa maana katika Isaka uzao wako utaitwa.
13 Naye mwana wa mjakazi nitamfanya kuwa taifa, maana huyu naye ni uzao wako.
14 Ibrahimu akaamka asubuhi na mapema akatwaa mkate na kiriba cha maji, akampa Hajiri akimtwika begani pake, na kijana, akamruhusu; naye akatoka, akapotea katika jangwa la Beer-sheba.
15 Yale maji yakaisha katika kiriba, akamlaza kijana chini ya kijiti kimoja.
16 Akaenda akakaa akimkabili, mbali naye kadiri ya mtupo wa mshale; maana alisema, Nisimwone kijana akifa; naye akakaa akimkabili, akapaza sauti yake, akalia.
17 Mungu akasikia sauti ya kijana. Malaika wa Mungu akamwita Hajiri kutoka mbinguni, akamwambia, Una nini, Hajiri? Usiogope, maana Mungu amesikia sauti ya kijana huko aliko.
18 Ondoka, ukamwinue kijana, ukamshike mkononi mwako, kwa kuwa nitamfanya kuwa taifa kubwa.
19 Mungu akamfumbua macho, naye akaona kisima cha maji; akaenda akakijaza kiriba maji, akamnywesha kijana.
20 Mungu akawa pamoja na huyo kijana, naye akakua, akakaa katika jangwa, akawa mpiga upinde.
21 Akakaa katika jangwa la Parani; mama yake akamtwalia mke katika nchi ya Misri.

Abraham à Beer-Shéba

22 Ikawa wakati ule Abimeleki, na Fikoli mkuu wa jeshi lake, wakamwambia Ibrahimu, wakinena, Mungu yu pamoja nawe katika yote unayotenda.
23 Basi sasa uniapie kwa Mungu, ya kuwa hutanitenda hila, wala mwanangu, wala mjukuu wangu, lakini kwa kadiri ya fadhili niliyokutendea utanitendea mimi, na nchi hii ambayo umetembea ndani yake.
24 Ibrahimu akasema, Nitaapa.
25 Kisha Ibrahimu akamlaumu Abimeleki kwa sababu ya kisima cha maji ambacho watumwa wa Abimeleki wamekinyang’anya.
26 Abimeleki akasema, Mimi sijui ni nani aliyetenda neno hili, wala hukuniambia, wala sikusikia habari hii ila leo tu.
27 Ibrahimu akatwaa kondoo na ng’ombe akampa Abimeleki, na hao wawili wakafanya mapatano.
28 Ibrahimu akaweka wana kondoo wa kike saba peke yao.
29 Abimeleki akamwambia Ibrahimu, Hawa wana kondoo wa kike saba, uliowaweka peke yao, maana yake nini?
30 Akasema, Hawa wana kondoo wa kike saba utawapokea mkononi mwangu, wawe ushuhuda ya kuwa ni mimi niliyekichimba kisima hiki.
31 Kwa hiyo akapaita mahali pale Beer-sheba, kwa sababu waliapa huko wote wawili.
32 Basi wakafanya mapatano huko Beer-sheba. Abimeleki, na Fikoli mkuu wa jeshi lake, wakaondoka wakarudi hata nchi ya Wafilisti.
33 Ibrahimu akapanda mkwaju huko Beer-sheba, akaliitia huko jina la Bwana Mungu wa milele.
34 Ibrahimu akakaa hali ya ugeni katika nchi ya Wafilisti siku nyingi.

Cette Bible est dans le domaine public.