Fermer le panneau de recherche

Appuyez sur Entrée pour rechercher ou ESC pour annuler.

2 Samuel 2.23
Bible en Swahili de l’est


Sacre de David et d’Ish-Bosheth

1 Ikawa baada ya hayo, Daudi akauliza kwa Bwana, akasema, Je! Niupandie mji wo wote wa Yuda? Bwana akamwambia, Haya! Panda. Daudi akasema, Niupandie mji upi? Akasema, Hebroni.
2 Basi Daudi akapanda aende huko, pamoja na wakeze wawili, Ahinoamu wa Yezreeli, na Abigaili, mkewe Nabali, wa Karmeli.
3 Daudi naye akawapandisha watu wake waliokuwa pamoja naye, kila mtu na watu wa nyumbani mwake; wakakaa katika miji ya Hebroni.
4 Basi watu wa Yuda wakaenda, wakamtia Daudi mafuta huko, awe mfalme juu ya nyumba ya Yuda. Wakamwambia Daudi wakasema, Watu wa Yabesh-gileadi ndio waliomzika Sauli.
5 Basi Daudi akatuma wajumbe kwa watu wa Yabesh-gileadi, na kuwaambia, Na mbarikiwe ninyi na Bwana, kwa kuwa mmemtendea bwana wenu fadhili hii, yaani Sauli, mkamzika.
6 Bwana naye sasa awatendee ninyi fadhili na kweli; mimi nami nitawalipeni fadhili hiyo, kwa sababu mmetenda jambo hilo.
7 Basi sasa, mikono yenu na itiwe nguvu, nanyi iweni mashujaa; maana Sauli, bwana wenu, amekufa, tena nyumba ya Yuda wamenitia mimi mafuta niwe mfalme juu yao.
8 Basi Abneri, mwana wa Neri, amiri wa jeshi la Sauli, alikuwa amemtwaa Ishboshethi, mwana wa Sauli, na kumvusha na kumpeleka Mahanaimu;
9 akamweka awe mfalme juu ya Gileadi, na Waasheri, na Yezreeli, na Efraimu, na Benyamini, na juu ya Israeli wote.
10 (Huyo Ishboshethi, mwana wa Sauli, umri wake alikuwa amepata miaka arobaini alipoanza kutawala juu ya Israeli, akatawala miaka miwili.) Lakini nyumba ya Yuda waliandamana na Daudi.
11 Na wakati Daudi alipotawala Hebroni juu ya nyumba ya Yuda ulikuwa miaka saba na miezi sita.
12 Basi Abneri, mwana wa Neri, na watumishi wa Ishboshethi, mwana wa Sauli, wakatoka Mahanaimu kwenda Gibeoni.
13 Huyo Yoabu naye, mwana wa Seruya, na watumishi wa Daudi, wakatoka, wakakutana nao karibu na ziwa la Gibeoni; wakaketi, hawa upande huu wa ziwa, na hawa upande huu wa ziwa.
14 Abneri akamwambia Yoabu, Tafadhali vijana hawa na waondoke na kucheza mbele yetu. Yoabu akasema, Haya! Na waondoke.
15 Basi wakaondoka, wakaenda upande wa pili kwa hesabu yao watu kumi na wawili wa Benyamini, na wa Ishboshethi, mwana wa Sauli na watu kumi na wawili wa watumishi wa Daudi.
16 Wakakamatana, kila mtu akimshika mwenziwe kichwa chake, na kutia upanga wake katika ubavu wa mwenzake; wakaanguka pamoja; hata mahali pale pakaitwa Helkath-hasurimu, napo ni katika Gibeoni.
17 Vita vile vilikuwa vikali sana siku ile; naye Abneri akashindwa, na watu wa Israeli, mbele ya watumishi wa Daudi.
18 Na wana watatu wa Seruya walikuwako huko, Yoabu, na Abishai, na Asaheli; na Asaheli alikuwa mwepesi wa miguu kama kulungu.
19 Naye Asaheli akamfuatia Abneri; na katika kwenda kwake hakugeuka kwenda mkono wa kuume wala mkono wa kushoto katika kumfuatia Abneri.
20 Basi Abneri akatazama nyuma yake, akasema, Ni wewe, Asaheli? Akajibu, Ni mimi.
21 Basi Abneri akamwambia, Geuka mkono wa kuume au mkono wa kushoto, ukamshike mmoja wa vijana, ukazitwae silaha zake. Lakini Asaheli hakukubali kugeuka na kuacha kumfuata.
22 Abneri akamwambia Asaheli mara ya pili, Geuka, acha kunifuatia mimi; kwa nini nikupige hata chini? Hapo ningewezaje kuinua uso wangu mbele ya Yoabu, ndugu yako?
23 Lakini akakataa kugeuka; kwa hiyo Abneri akampiga tumboni kwa ncha ya nyuma ya mkuki wake, ule mkuki ukamtoka kwa nyuma; naye akaanguka hapo, akafa papo hapo; ikawa, watu wote waliofika hapo, alipoanguka Asaheli na kufa, wakasimama.
24 Ila Yoabu na Abishai wakamfuatia Abneri; na jua likachwa hapo walipoufikilia mlima wa Ama, uelekeao Gia, katika njia ya nyika ya Gibeoni.
25 Nao wana wa Benyamini wakakusanyika pamoja nyuma ya Abneri, wakawa kikosi kimoja, wakasimama juu ya mlima.
26 Ndipo huyo Abneri akamwita Yoabu, akasema, Je! Upanga uwale watu sikuzote? Je! Hujui ya kwamba utakuwa uchungu mwisho wake? Basi itakuwa hata lini usijewaamuru watu warudi na kuacha kuwafuatia ndugu zao?
27 Naye Yoabu akasema, Aishivyo Mungu, usingalinena, basi asubuhi wangalikwenda zao, wasiwafuatie kila mtu ndugu yake.
28 Basi Yoabu akapiga tarumbeta, na watu wote wakasimama, wasiwafuatie Israeli tena, wala hawakupigana tena.
29 Wakaenda Abneri na watu wake usiku ule wote kati ya ile Araba; wakavuka Yordani, wakapita kati ya Bithroni yote, wakaja Mahanaimu.
30 Akarudi Yoabu naye kutoka kumfuatia Abneri; na alipokwisha kuwakusanya watu wote pamoja, wa hao watumishi wa Daudi walipungukiwa na watu kumi na kenda pamoja na Asaheli.
31 Ila watumishi wa Daudi walikuwa wamewapiga watu wa Benyamini, na watu wa Abneri, hata wakafa watu mia tatu na sitini.
32 Nao wakamwinua Asaheli, wakamzika katika kaburi la baba yake, lililokuwako Bethlehemu. Yoabu na watu wake wakaenda usiku kucha, wakapambazukiwa huko Hebroni.

Cette Bible est dans le domaine public.